Thursday, September 20, 2012

RATIBA YA UCHAGUZI MDOGO WA MADIWANI KATIKA KATA 29 NNCHI NZIMA

WAKATI Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), ikitangaza chaguzi ndogo za madiwani katika kata 29 za Halmashauri 27 nchini utakaofanyika Oktoba 28, mwaka huu, viongozi wa vyama vya upinzani wamelalamika wakisema imeshindwa kusimamia uchaguzi huru na wa haki.
Akizungumza katika mkutano na viongozi wa vyama vya siasa, Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Damian Lubuva amesema ratiba ya uchaguzi hiyo imeshatolewa na kwamba tume hiyo imejiandaa vya kutosha kuhakikisha uchaguzi huo unafanikiwa.
“Tume tayari imekwisha toa ratiba nzima ya chaguzi hizi kuanzia siku ya kupiga kura. Tunatarajia vyama vya siasa vitakavyoshiriki  chaguzi hizi pamoja na wadau wengine watazingatia ratiba hii na kuifuata kwa makini ili kuepusha usumbufu utakaoweza kujitokeza endapo ratiba itakiukwa,” alisema Jaji Lubuva. Licha ya kutaja hatua ya wapiga kura kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura, Jaji Lubuva alisema daftari litakalotumika ni lile la mwaka 2010 na kwamba daftari hilo litarekebishwa kabla ya mwaka 2015. Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa tume hiyo, Julius Malaba fomu za uteuzi wa wagombea zimeanza kutolewa na wasimamizi wa uchaguzi kuanzia jana (juzi) Septemba 19, 2012 na zitaendelea kutolewa hadi Oktoba 2, 2012 kuanzia saa 1.30 asubuhi hadi 9.30 alasiri siku za kazi.

Malalamiko ya vyama vya siasa
Wakitoa maoni hayo katika mkutano huo, viongozi wa vyama vya siasa waliikosoa Tume hiyo wakisema imeshindwa kusimamia chaguzi nchini.
Mwenyekiti wa Chama cha National League for Democracy, Dk Emmanuel Makaidi alisema utendaji wa Tume hiyo ni mbovu ndiyo maana baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 kumekuwa na kesi nyingi za kupinga matokeo,
“Kama kuna tume inayofanya madudu basi ndiyo hii, ilifanya hivyo kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ndiyo maana kuna kesi 47 za kupinga matokeo,” alisema Dk Makaidi na kuongeza:
“Tume ile ilishiriki katika kuchakachua uchaguzi… sioni ajabu Mwenyekiti na mkurugenzi kuondolewa.. ikiendelea hivi nchi itaingia vitani na Nec itawajibika,”
Naye Kaimu Katibu mkuu wa UDP, Isaac Cheyo alisema tume hiyo haina nguvu ya kusimamia sheria na maadili yaliyopo,
“Umesema maadili yanakataza vyama kutoa lugha chafu, kama ikitokea mlalamikaji aende kwenye kamati ya maadili inayoongozwa na Katibu tawala wa mkoa na wilaya na katibu tarafa. Hawa hawana mamlaka ya kushughulikia,” alisema Cheyo.
Aliongeza kuwa licha ya daftari la kudumu la wapiga kura kupitiwa, mchakato wake haukuwashirikisha wananchi.
“Ni Daftari bovu, mwaka 2009, Serikali ilifanya mabadiliko ya vijiji na kata. Ilipofika wakati wa uchaguzi mtu amejiandikishia kata Fulani, anaambi wa jina liko kata nyingine…” alisema.
Naye Mkurugenzi wa uchaguzi wa Chadema, Msafiri Mtemelwa alisema tatizo la Nec ni kutokuwa na mtandao nchi nzima badala yake inatumia maofisa wa Serikali.Aliongeza kuwa mfumo mzima wa uchaguzi unalenga kukinufaisha CCM na kuvikandamiza vyama vya upinzani,“Tatizo sijui CCM wanataka watawale milele… kuna kata 12 nchini hazijafanya uchaguzi mwaka mzima. CCM wanaangalia kama watashinda, wakiona wanashindwa wanamwambia Waziri wa Tamisemi aahirishe uchaguzi…” alidai Mtemelwa.
 Naye mwakilishi kutoka NCCR Mageuzi, Faustine Sungura aliitaka Tume hiyo kuwalipa mawakala wa vyama vya siasa kama vile inavyowaapisha kutunza siri zake,“Ki uhalisia mimi mgombea sina wakala, kwa sababu unamwapisha  ili atunze siri za tume, mmeshamchukua. Basi muwalipe,” alisema Sungura.
Akijibu  maoni hayo, Jaji Lubuva alisema tangu ameingia katika tume hiyo amekuwa na nia ya kuona tume hiyo inakuwa huru lakini bado Serikali haijatekeleza maombi yake. “Tangu nilipoapishwa kushika nafasi hii, nia yangu ni kutatua kasoro hizo.. lakini hiyo ni kazi ya Serikali, kwa mfano hilo la kuwa na mtandao nchi nzima wanasema leteni bajeti,” alisema Jaji Lubuva na kuongeza:
“Nilipokwenda kujitambulisha Zanzibar, Rais aliuliza, mbona hamna ofisi?..Hayo ya uhuru wa tume tumeshayazungumza sana, lakini wakati wa kutangaza mshindi, hawa wajumbe wote wanahusika siyo mtu mmoja.”

No comments:

Post a Comment