Saturday, February 2, 2013

Wanafunzi wa kike watumia mtandao kujiuza

PENGINE haya tunaweza kuyaweka kwenye kundi la madhara yatokanayo na utandawazi. Mitandao ya kijamii ipo inayowasaidia wanafunzi katika masomo yao na kazi, lakini wengine wanatumia mitandao hiyo visivyo.
 
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa matumizi mabaya ya teknolojia hasa mitandao ya kijamii yamechochea ongezeko la uhalifu, ubakaji, matumizi ya dawa za kulevya na zaidi biashara ya ukahaba vyuoni.
Mitandao ya ‘Facebook’, ‘Twitter’, ‘BBM’, ‘Instagram’ inafahamika kwa namna inavyoweza kuwaunganisha watu kutokana na urahisi wake katika kuitumia.
Mwananchi Jumapili limebaini kuwa katika mitandao hiyo makundi mbalimbali yameanzishwa yakiwa na malengo tofauti.
Baadhi wameanzisha makundi kwa lengo la kujenga mitandao ya kibishara, kidini, michezo, burudani, vichekesho na mengine ambayo mara nyingi huwa wazi na yeyote anaweza kujiunga na kuona kinachoendelea ndani.
Mbali na hayo ndani ya mtandao wa ‘Facebook na ‘BBM’ yapo makundi yanayoendesha biashara ya ukahaba, yakiwahusisha wanafunzi wa vyuo vikuu mbalimbali nchini.
Uchunguzi umebaini kuwa wanafunzi hao wanaofanya biashara ya ukahaba kwa kutumia mitandao wameweka picha na namba kwa ajili ya mawasiliano kwa mteja atakayekubaliana na bei waliyoweka.
Baadhi ya wanafunzi hao wanatumia mtandao wa ‘University Tanzania  Jokes’, ‘Jicho la Mvulana Liko Fasta Kuliko Google’, ‘Benki ya Utamu Tanzania’ na nyingine katika kufanikisha biashara hiyo ya ngono.
Ukiingia katika mitandao ya Facebook, Twitter, BBM, Instagram, utabaini kuwapo kwa makundi yaliyoundwa kutengeneza mitandao ya ngono, ambayo huweka pia namba za  simu za wahusika, zikiambatana na picha, ambao ikiwa utaangalia picha na kuvutiwa, unaweza ukapiga simu husika kuzungumza naye kwa kufanya mapatano kabla ya kukubaliana.
Uchunguzi wa Mwananchi Jumapili umebaini kuwa mwanamume anaweza kumpata msichana kutoka chuo kikuu chochote nchini anayefanya biashara ya ukahaba kupitia mitandao hiyo.
Baadhi ya vyuo wanavyotoka wasichana wanaofanya biashara hiyo na kujitangaza kwenye mitandao ni pamoja na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT), Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) na Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM).
Kwa nyakati tofauti, waandishi wa gazeti hili walitembelea makundi yanayojinadi kufanya biashara hiyo pamoja na kufanya mawasiliano na wasichana watatu ambao waliweka picha na namba zao kwenye mtandao.

Wasichana hao walijitambulisha kwa majina, vyuo na vitivo wanavyosoma na baada ya kuwafuatilia kwa kuweka ahadi za kimapenzi ilithibitika kuwa wanafanya biashara ya ukahaba huku wakiwa wanafunzi wa vyuo vikuu.
Mmoja wa wasichana hao alijitambulisha kwa jina la Bianca (sio jina lake halisi), ambaye ni mwanafunzi wa mwaka wa pili Kitivo cha Sheria, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Baada ya mwandishi kufanya naye mawasiliano walikubaliana kukutana eneo la Udasa na muda wa ahadi ulipofika, mwandishi alifika eneo hilo na kukutana na binti huyo ambaye aliiona picha yake na namba ya simu kwenye mtandao, tofauti na alivyodhani awali kuwa huenda wasichana hao wanatumia picha za watu wengine kujinadi.
Kutokana na lengo la msichana kuwa ni biashara ya ngono, mwandishi wa gazeti hili alilazimika kumpeleka binti huyo katika hoteli moja maarufu jijini, akimweleza kuwa inabidi wanywe pombe kwanza kabla ya kwenda chumbani kwa makubaliano ya kumlipa Sh50,000.
Binti huyo alikabidhiwa fedha hizo ili kumwaminisha uhalisia wa kuwapo hitaji na muda wa kwenda naye chumbani ulipofika waliongozana lakini mwandishi akatoroka  njiani akiwa amethibitisha kuwapo kwa tabia hiyo.
Gazeti hili lilimfuatilia mwanafunzi mwingine ambaye alijitambulisha kuwa anasoma katika Chuo cha Ustawi wa Jamii, ambaye kama ilivyokuwa kwa wa kwanza, hakupata taabu kujieleza.
Baada ya mwandishi kueleza alipoipata namba yake mazungumzo yao yalikuwa hivi:
Binti aliuliza: “...Kwa hiyo, uko wapi?”
Mwandishi alijibu:  “Nipo Ubungo.”
Binti akauliza tena: “Unaweza kuja Ustawi?”
Baada ya mawasiliano hayo mwandishi aliambiwa binti huyo kuwa anaweza kumfuata chuoni hapo.
Mwandishi wa gazeti hili alifika maeneo ya Kijitonyama jirani na kilipo chuo hicho, na kumpigia simu binti huyo, ambaye aliipokea na safari hii alimwambia mwandishi kuwa ikiwezekana aje na rafiki yake.
Ilichukua nusu saa kwa wasichana hao kufika katika baa, ambayo mwandishi alikaa kuwasubiri, mara walitokea wasichana hao wakiwa wachangamfu, warembo waliovalia mavazi ya kisasa, yaliyoacha sehemu kubwa ya miili yao wazi.
Muda wa dakika saba walizokaa zilitosha kuwafanya wazoeane na mwandishi kama vile waliwahi kukutana miaka mingi ya nyuma, stori, vinywaji na mambo yalifanyika  kama ilivyokuwa Udasa.
Mwananchi Jumapili liliendelea na uchunguzi wake kwa wasichana wengine ambao wameweka picha zao katika mitandao hiyo wakijiuza, ambapo walipopigiwa simu walijibu na kufika katika maeneo waliyokubaliana.
chanzo-Mwananchi

No comments:

Post a Comment