Sunday, November 3, 2013

Vita ya Lema na Zitto yafika pabaya

Dar es Salaam. Vita vya maneno kati ya Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe imefika pabaya.
Vita hiyo ya maneno iliyoanzishwa na Lema katika kikao cha wabunge wiki iliyopita kwamba Zitto anafanya unafiki kukataa posho, jana iliingia katika hatua nyingine baada ya mwakilishi huyo wa Arusha kumshushia tuhuma Mbunge huyo wa Kigoma Kaskazini kwamba anakataa posho za vikao bungeni, lakini anapokea posho nyingi kutoka mashirika mbalimbali ya kijamii nchini.
Lema aliweka tuhuma hizo kwenye Mtandao wa Jamii Forum huku akisema kuwa, suala hilo halihitaji vikao vya chama kulijadili isipokuwa vyombo vya habari na hususani mitandao ya kijamii kwani hata Zitto hutumia mitandao hiyo.
Katika hoja yake, Lema alisema kuwa Zitto ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) anakataa posho ya Sh70,000 kwa kikao kimoja cha Bunge, lakini anapokea Sh700,000 mpaka Sh1,000,000 kwa kikao kimoja cha kamati yake na haswa vile vinavyoandaliwa na mifuko ya jamii.
Hata hivyo, zitto alikanusha shutuma hizo akimtaka Lema kutoa ushahidi kama kuna mjumbe yoyote wa kamati ya PAC anayepokea posho, huku akieleza kuwa hawezi kubishana na Mbunge huyo wa Arusha mjini kwani yeye Zitto ni kiongozi wake ndani ya Chadema.
“Naomba kutaja masilahi yangu katika hili, wabunge wa kawaida wakialikwa katika vikao hivyo huwa wanalipwa Sh500,000 kwa kikao kwa siku . Mimi nimewahi kuhudhuria vikao hivyo mara mbili na nikalipwa hivyo pamoja na chai na chakula cha mchana.” alisema Lema.
Lema alisema posho hizo za wabunge ni tofauti na zile za Mwenyekiti wa PAC kwani yeye pamoja na posho ya Sh700,000 mpaka Sh1,000,000 hupewa mafuta ya gari au tiketi ya ndege ya kumtoa alipo na kumrudisha na kukodiwa hoteli yenye hadhi ya nyota nne mpaka tano ambayo kwa siku gharama yake ni Dola za Marekani 100 mpaka 600 kwa siku .
Akijibu hoja hizo, Zitto alisema tangu siku nyingi alikwisha piga marufuku kwa PAC kupokea posho kutoka taasisi au mashirika yanayosimamiwa na kamati hiyo.
“Toka nimekuwa Mwenyekiti wa POAC (Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma) sio tu nilipiga marufuku posho bali pia niliwashitaki PCCB (Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa) wabunge wanaochukua posho kutoka kwa taasisi za Serikali,” alisema Zitto.
Alieleza baada ya hatua hiyo, wabunge walihojiwa na PCCB kuhusu jambo hilo mpaka aliyekuwa Spika wa Bunge wakati huo, Samuel Sitta alipoingilia kati na kuwatetea wabunge hao.
“Hiyo ilikuwa mwaka 2009 kabla hata Lema hajawa mbunge, wajumbe wa kamati ya PAC wanalipwa posho za vikao kama wabunge wengine, lakini mimi sichukui posho hizo za vikao,” alisema na kuongeza:.
“Sio tu PAC hata kwenye Baraza la Madiwani na Baraza la Mashauriano la Mkoa wa Kigoma na popote kule. Hata NGO (Mashirika yasiyo ya Kiserikali) zikinialika kwenye vikao vyao sichukui posho za vikao. Nafasi yoyote ninayoalikwa kama mbunge sichukui posho za vikao,” alisema Zitto.

No comments:

Post a Comment