Wednesday, November 20, 2013

Afrika Kusini yasitisha uokoaji kwa muda

Kikosi cha waokoaji katika jengo lililoporomoka Tongaat, Afrika Kusini.
Jitihada za uokoaji zimesitishwa kwa muda baada ya paa la jengo la maduka lililokuwa linajengwa kuporomoka nchini Afrika Kusini.
Msemaji wa Polisi Thulani Zwane ameiambia BBC kwamba kazi ya kuwatafuta watu walionusurika itaanza tena baada ya kuondoa baadhi ya matofali.
Mtu mmoja ameripotiwa kufa na wengine 40, wengi wao wakiwa ni mafundi wa ujenzi wanahofiwa kukwama katika kifusi katika eneo la ujenzi la Tongaat, kaskazini mwa Durban.
Watu wapatao 30 wameokolewa, baadhi yao wakiwa katika hali ya taharuki.
Kepteni Zwane amesema watu 11 miongoni mwa waliopelekwa hospitali wamejeruhiwa vibaya.
Naibu meya wa mji wa Tongaat ameviambia vyombo vya habari vya Afrika Kusini kuwa serikali ilipata amri ya mahakama mwezi mmoja uliopita, kusitisha ujenzi katika eneo la Tongaat, ambao ni mji mdogo uliopo kilomita 40 kaskazini mwa Durban.

No comments:

Post a Comment