Wednesday, November 20, 2013

Cameroon yazifuata Nigeria, Ivory Coast

Cameroon imekuwa nchi ya tatu kutoka barani Afrika kufuzu kucheza kombe la dunia nchini Brazil mwaka kesho 2014 baada ya kuifunga Tunisia siku ya jumapili kwa magoli 4 - 1 katika mechi iliyopigwa mjini Younde Cameroon.
Cameroon itashiriki fainali hizo za Kombe la Dunia kwa mara ya sita tangu mashindano hayo yalipoanza ambapo sasa itaungana na Nigeria na Ivory Coast ambazo nazo zimefuzu kushiriki mashindano hayo.
Sherehe ya Cameroon ilianza kipindi cha kwanza baada ya Pierre Webo na Benjamini Moudandjo kupachika magoli.
Hadi kipindi cha kwanza kinamalizika Cameroon walikuwa na jumla ya magoli 2 - 0.
Kipindi cha pili kilianza kwa kushambuliana kwa zamu ambapo Tunisia waliapachika goli katika dakika ya 50 lililofungwa na Ahmed Akaichi anachezea Esperance.
Hata hivyo Cameroon hawakukata tamaa na waliendelea kucharuka na hatimaye wakajipatia goli la tatu lililofungwa na Jean Makoun kabla ya kuziba ndoto za Tunisia ambapo zikiwa zimebaki dakika tatu mpira kumalizika Jean Makoun akaongeza ladha kwenye sherehe ya Cameroon pale alipopachika goli zuri la nne baada ya mabeki wa Tunisia kujichanganya.
Hadi mpira unamalizika Cameroon wakaondoka kifua mbele kwa kuipachika Tunisia jumla ya magoli 4 - 1
Kwa matokeo hayo sasa Cameroon inaungana na Nigeria na Ivory Coast ambazo nazo tayari zimeshajihakikishia kwenda nchini Brazil kushiriki fainali za Kombe la dunia mwaka 2014.

No comments:

Post a Comment