Friday, November 15, 2013

Lulu kuweka taarifa za filamu zake kwenye simu

Dar es Salaam. Mwigizaji Bora wa Kike kwa mujibu wa tuzo za Tamasha la Majahazi la mwaka huu, Elizabeth Michael maarufu kwa jina la Lulu,  amesema anatarajia kuanza kutoa taarifa zote zinazohusiana na filamu zake kupitia simu za mkononi.
 
Akizungumza na Mwananchi jana Lulu alisema taarifa hizo zitapatikana kupitia mitandao yote ya simu za mkononi hapa nchini. “Shabiki wangu pia anaweza kuangalia filamu zangu kupitia mitandao ya kijamii yaani Tigo, Zantel, Vodacom na Airtel. Bado haijawa rasmi hivyo nitakapozindua ndipo nitakapotoa mwongozo halisi,” alisema Lulu.
Kwa mujibu wa Lulu bado hajajua ni lini bidhaa yake hiyo itaanza kurushwa hewani ila kwa sasa yupo katika mazungumzo ya mwisho na wadau wa mitandao ya simu za mikononi.
“Hii ni moja ya mafanikio katika tasnia ya filamu hivyo siwezi nikasema ni lini mpango huu utaanza kurushwa hewani na mashabiki kupata huduma hii, ila natarajia kesho (leo) nitaweza kutoa taarifa rasmi ni lini sasa mashabiki waanze kujiunga na huduma hii.”
Miezi michache iliyopita Lulu alizindua filamu yake mpya Foolish Age katika ukumbi wa Mlimani City, filamu inayofanya vizuri sokoni kwa hivi sasa. Hata hivyo Lulu ni kati ya hazina na vipaji vilivyokuzwa tangu utotoni ambapo anaonyesha kuliteka soko kwa sasa na huenda anaweza kuwapiku wasanii wakubwa wa kike hapo baadaye.

No comments:

Post a Comment