Friday, September 7, 2012

CHADEMA wasitisha M4C kwa muda

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimetangaza kusitisha kwa muda Operesheni ya Vuguvugu la Mabadiliko (M4C) mkoani Iringa na badala yake kimeitisha kikao cha Kamati Kuu cha dharura kujadili mfululizo wa mauaji yanayofanywa na polisi katika mikutano yao.
Mkuu wa oparesheni hiyo iliyopangwa kufanyika mikoa mitano, Benson Kigaila, jana aliwaambia waandishi wa habari mjini Iringa kuwa wamelazimika kukutana kujadili hatua zaidi za kuchukua.
Alisema kamati kuu itakutana jijini Dar es Salaam Jumapili hii na kutoa tamko juu ya nini kifanyike baada ya wao kuwasilisha taarifa nzima juu ya matukio mbalimbali yaliyotokea kuanzia siku ya kwanza ya operesheni hiyo.
“Tunahitaji kukaa na kutafakari juu ya matukio haya kwa kuwa si jambo la kawaida, polisi waue watu kwenye mikutano, nasi tukaendelea na mikutano yetu bila kuchukua hatua stahiki,” alisema.
Alisema wakati wote tangu kuanzia kutokea kwa msiba wa Mwangosi, kumekuwa na propaganda nyingi zilizojitokeza juu ya hali hiyo, huku serikali, polisi na CCM wakitaka kuhamishia lawama kwa CHADEMA.
Kigaila aliongeza kuwa Watanzania wanajua kuwa mikutano na maandamano ambayo polisi hawaingilii kuvunja haileti misukosuko wala vifo, kama ilivyokuwa kwenye mikoa mbalimbali, ikiwamo ya Lindi na Mtwara.
Alisema wananchi wanapaswa kutambua kwamba kuna kitu cha ziada ambacho serikali ya CCM na Jeshi la Polisi wanakifanya dhidi ya CHADEMA, na si shughuli ya sensa ambayo imegeuzwa sababu ya kusitisha mikutano yao, kwani wakati serikali inazuia CHADEMA kufanya kazi zake, CCM inaendelea na mikutano na mchakato wa uchaguzi.

No comments:

Post a Comment