Wednesday, October 16, 2013

Zitto avitikisa vyama vya siasa ni kwa kuagiza ruzuku isitishwe.

Nape alifafanua kwamba hesabu za 2011/2012 bado ziko kwa wakaguzi wa nje, wakishakamilisha nazo zitawasilishwa kwenye vikao vya chama na hatimaye kwa CAG.
“Hesabu hizi zikikaguliwa kwa mujibu wa utaratibu, anapelekewa CAG ambaye ndiye anazipeleka kwa Msajili wa Vyama vya Siasa na sio vinginevyo,” alisema.
Alidai kuwa Zitto anapaswa kuanza kutoa ‘boriti kwenye jicho lake ndipo aone kibanzi kwenye jicho la mwenzake’ kwa sababu chama chake ndicho kimekuwa na matumizi mabaya ya ruzuku. Alisema Zitto kama Naibu Katibu Mkuu wa Chadema ni vyema akawajibika ndani ya chama chake ili kuonyesha mfano kwa wengine.
“Wote tunakumbuka kelele zilizopo mtaani kuhusu matumizi mabaya ya ruzuku zinazoelekezwa na Chadema na viongozi wake kutoka kwa wanachama wao, hivyo si ajabu wakawa wanakiuka sheria hii na ndiyo chanzo cha kelele hizo za wanachama wao,”alisema.
Vyama vingine
Kwa upande wake, Chadema kilieleza kwamba hakijapata barua inayowaarifu kuhusu kutaka kufungiwa ruzuku kutokana na kutowasilisha taarifa ya ukaguzi.
Ofisa Habari Mwandamizi wa Chadema, Tumaini Makene ilisema hata barua ya kuitwa kwenye Kamati ya PAC, iliwafikia kwa kuchelewa. “Tunasubiri barua rasmi ya suala hili ndio mamlaka zinazohusika na masuala ya fedha ndani ya chama, hususan, Baraza la Wadhamini wa Chama kuweza kutafakari hatua,” alisema Makene.
Hata hivyo, alisema angependa umma utambue kwamba “Chadema ndicho kilichokuwa mstari wa mbele tangu kabla na baada ya mwaka 2009 kutaka ukaguzi na wazi katika mapato na matumizi ya vyama vya siasa.”
Alifafanua kuwa msimamo wa Chadema kwenye mkakakati huo ulikuwa ni kuibana CCM kutokana na madai ya baadhi ya vigogo wake “kukwapua fedha Benki Kuu ( Akaunti ya Madeni ya Nje – EPA) na kuzitumia kwenye uchaguzi wa mwaka 2005.”
Alijigamba kuwa hesabu za chama chake zimekuwa zikikaguliwa kila mwaka na kwamba wanasubiri maelezo ya barua kuhusu kile kinacholalamikiwa.
Kwa upande wa Chama cha Wananchi (CUF) kimesema hesabu zake ziko safi, ila imeshindikana kukaguliwa kwa vile Serikali haijatoa fedha za kugharimia ukaguzi huo.
Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Tanzania Bara, Julius Mtatiro alisema hesabu zao zimekwishakaguliwa na wakaguzi wa ndani.

No comments:

Post a Comment