Sunday, October 20, 2013

TAHADHARI KWA WATUMIAJI WA KOMPYUTA ZENYE WINDOW XP


 

Watumiaji wa  programu ya komputa iitwayo Window XP wamepewa tahadhari na kampuni ya Microsoft ambayo ndiyo iliyotengeneza program hiyo kuwa hapatakuwa na matoleo mapya (updates) zaidi kuhusu Window XP Service Pack 3 baada ya mwezi wa nane mwaka 2014.

Akizungumza na wataalamu mbalimbali wa masuala ya ulinzi mtandao Agosti 16,mwaka huu Mkurugenzi wa kitengo kijulikanacho kwa jina la Microsoft Trustworthy Computing,Tim Rains anasema kuwa ingawa Window XP wakati inatolewa ilikuwa na ubora huku ikipendwa na watumiaji wengi wa kompyuta,kwa sasa imeonekana kuwa dhaifu kutokana na kuongezeka kwa uhalifu wa kimtandao.

Amesema kumekuwepo na wimbi kubwa la wahalifu wanaotumia mianya mbalimbali kuingilia kompyuta za wateja wanaotumia Window XP na kuongeza kuwa hali hiyo ya uhalifu itaendelea hasa kwa wale wataoendelea kutumia aina hiyo ya window.

Rains amesema wanaendelea kutafuta ufumbuzi pale itakapobainika wahalifu wameweza kupenya katika kompyuta za wateja wao wanaotumia aina mpya za window ambapo kwa sasa kupitia kituo cha kuangalia usalama wa kompyuta cha kampuni hiyo kinaendelea kutoa maelezo ya jinsi ya kuwalinda wateja wao.

Amesema kampuni ambazo bado zitakuwa zinatumia Window XP,zitasababisha wahalifu kutafuta mapungufu katika window hiyo na kuleta athari ambapo kampuni ya Microsoft haitakuwa na msaada ama wa bure au wa kulipia dhidi ya hali hiyo,kwani itakuwa imeshaacha kutoa msaada wa kuhusu Window XP


Chanzo:Gazeti la Mwananchi

No comments:

Post a Comment