Thursday, October 24, 2013

NI KWELI AU CHANGA LA MACHO KAMA KAWAIDA YA CCM

Dar es Salaam. Serikali inatarajia kuandaa hati ya dharura ili kuwezesha kufanyika kwa maboresho ya Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Mabadiliko ya Katiba ambayo yatajadiliwa upya katika Mkutano wa Bunge unaoanza Oktoba 29 mjini Dodoma.
 
Tayari vyama vya upinzani na chama tawala vimekubaliana taratibu muhimu za kufuata ili maboresho hayo yaweze kupita ndani ya Bunge. Muswada huo haukuwa umepangwa kujadiliwa katika mkutano ujao wa Bunge ndio maana itabidi iombwe hati hiyo ya dharura. Hatua hiyo ni ushindi kwa vyama vitatu vya upinzani vya Chadema, CUF na NCCR- Mageuzi, ambavyo vilipinga muswada huo wakati wa mkutano uliopita wa Bunge Septemba, mwaka huu.
Muswada wa sheria hiyo uliopitishwa Septemba na Bunge ulisusiwa na wabunge wa vyama hivyo wa upinzani kwa maelezo kuwa una kasoro kwenye baadhi ya vipengele.
Hata hivyo, wabunge wa CCM waliamua kuendelea na mjadala na kupitisha muswada huo kitendo ambacho kilisababisha mvutano mkubwa uliomfanya Rais Jakaya Kikwete kukutana na viongozi wa vyama vya siasa vyenye wabunge kumaliza tofauti zao.
Mbatia asoma tamko la vyama
Akisoma tamko la vyama vya siasa mbele ya waandishi wa habari jana, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia alisema hatua ya Serikali itakuja baada ya vyama vya siasa kufikia mwafaka wa vipengele vinavyotakiwa kufanyiwa marekebisho kwenye muswada huo. Mbatia alisema kuwa tayari kazi hiyo imefanyika na mapendekezo yao yameshapelekwa serikalini ingawa hakutaka kuingia kwa undani walichopendekeza katika marekebisho hayo.
Vyama vilivyokutana ni pamoja na CCM, Chadema, CUF, NCCR -Mageuzi, TLP. Pia vyama vya UDP na UPDP vilishiriki kwa niaba ya vyama visivyo na wabunge.
Mbatia alisema hatua inayofuata ni vyama kuunda kamati yao na Serikali kuunda yake ili kukubaliana kwa pamoja maeneo muhimu ya marekebisho.
Alisema lengo la hatua hiyo ni kuufanya mchakato wa Katiba kuwa shirikishi baada ya kamati hizo kumaliza kazi yake.
“Baada ya hapo, Serikali itaandaa hati ya dharura ili marekebisho yapelekwe haraka katika Mkutano wa Bunge unaoanza Oktoba 29, “ aliongeza Mbatia.
Mbatia alisema wanataka kabla ya Bunge la Katiba halijaanza basi sheria husika ifanyiwe marekebisho. “Tunawaomba Watanzania hasa wabunge waunge mkono juhudi hizi za vyama na Serikali ili kuhakikisha mchakato wa Katiba Mpya unakuwa shirikishi. Wabunge waridhie marekebisho haya na kuyapitisha,” alisema mbunge huyo wa kuteuliwa na Rais.

No comments:

Post a Comment