Saturday, July 13, 2013

Vita kali Chadema, CCM

Vyama vya CCM na Chadema vimekuwa vikituhumiana kuhatarisha amani ya nchi
Dar es Salaam. Siku tatu baada ya Rais Jakaya Kikwete kuponda mpango wa Chadema kuanzisha kambi kwa ajili ya mafunzo ya ulinzi kuwalinda viongozi na wanachama wake,  chama hicho kikuu cha upinzani nchini kimeibuka na kusema kuwa kinaendelea na mpango huo na kambi hizo zitaanza rasmi wiki ijayo.
Kimesema hakitishwi na kauli ya Jeshi la Polisi kukionya juu ya  uanzishwaji wa mafunzo hayo,  kwamba jeshi hilo linatakiwa kuanza kukizuia Chama Cha Mapinduzi (CCM)  kwanza, kwa maelezo kuwa chama hicho tawala pia kina kikundi cha ulinzi ‘Green Guards’ ambacho kinafanya mafunzo ya kijeshi, huku kikitumia silaha za moto.
“CCM ndiyo wataipeleka nchi hii pabaya, wanawafundisha vijana huku wakiwabebesha  bunduki, wanajenga taifa la aina  gani, bunduki ni silaha ya kivita sasa wanaandaa watu kupigana na nani” alisema Mkurugenzi wa Organaizesheni na Mafunzo wa chama hicho, Benson Kigaira jana wakati akizungumza na wanahabari huku akionyesha picha za mafunzo ya CCM, zinazoonyesha vijana wakiwa wamebeba silaha (hata hivyo ni mbao zilizotengenezwa kwa mfano wa bunduki).
Wakati Chadema wakieleza hayo, CCM kimeshtushwa na taarifa hizo na kueleza kuwa hali hiyo sasa inahatarisha usalama wa nchi.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa chama hicho (UVCCM), Martin Shigela alisema ni vyema Chadema kikawaambia wananchi wawalinde, kuliko kuanzisha mafunzo huku akimtaka Msajili wa Vyama vya siasa nchini, John Tendwa kulitizama kwa kina suala hilo.
Akifunga Kongamano  la Amani lililoandaliwa  na Kituo cha Demokrasia  Tanzania (TCD), Dar es Salaam Julai 10, mwaka huu, Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Taifa pia alikosoa kitendo cha Chadema kususia kongamano hilo alisema, “Sasa hawa kweli wanapenda amani yetu wakati hawapendi tuzungumze wanataka watu wauane, wapigane.”
Mbali na Rais Kikwete, Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, SSP Advera Senso juzi alikionya chama hicho kuhusu mpango huo akisema kuwa kitendo cha chama chochote cha siasa kikiwemo Chadema, kuanzisha kikundi cha kujihami ni kinyume na sheria za nchi na endapo watafanya hivyo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
Kauli ya jana ya Chadema ni mwendelezo wa ile iliyotolewa na Mwenyekiti wa chama hicho Freeman Mbowe Julai 9, mwaka huu, ambapo alisema  kimechukua hatua hiyo baada ya Serikali na vyombo vyake vya ulinzi na usalama kushindwa kufanyia kazi malalamiko yao kuhusu mauaji, vitisho na matukio ya kutisha wanayofanyiwa baadhi ya viongozi na wanachama wao.
Katika ufafanuzi wake Kigaila alisema Chadema hakianzishi vikundi vya kijeshi, bali mafunzo ya  kuwafundisha walinzi wa chama hicho  ‘Red Brigade’, jinsi ya kujilinda.
“Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni haki kwa raia yeyote kujilinda, Chadema ni taasisi ni haki yetu kuilinda taasisi yetu ndiyo maana tumesajili kikundi chetu cha ulinzi, sasa nani anatutisha, tunataka polisi waanze na CCM kwanza ambao katika mafunzo yao  wanafundisha hadi kupiga saluti na kutumia silaha,” alisema.
Alisema mafunzo hayo yataanza rasmi wiki ijayo, huku akisita kutaja siku yatakayoanza, wala mikoa yatakayofanyika na kusisitiza kuwa hayo yatatangazwa wiki ijayo wakati vijana wakienda katika mafunzo.

Sunday, June 9, 2013

Warioba: Ikulu kugawanywa

Dar es Salaam: Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema iwapo Mfumo wa Serikali Tatu utaridhiwa na wananchi ni lazima mambo yaliyo ndani ya Muungano yatagawanywa ikiwa ni pamoja na Ikulu ya Rais.
Amesema kuwa kutokana na taifa kufanya mabadiliko ya Katiba ni lazima kuwepo mpangilio wa kugawana mambo mbalimbali yaliyokuwa chini ya Muungano ikiwamo majengo, wafanyakazi, Ikulu, hata vitendea kazi na kwamba utaratibu huo ni kama ule uliotumika wakati Tanganyika na Zanzibar zilipoungana.
Kauli ya hiyo ya Jaji Warioba imekuja siku tatu tangu Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe kueleza kuwa Tanzania Bara itaanza mchakato wa kutunga Katiba yake Aprili mwaka 2014 na kumalizika Desemba mwaka huohuo.
Jaji Warioba aliyasema hayo katika mahojiano maalumu na waandishi waandamizi wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), inayochapisha magazeti ya Mwananchi, Mwananchi Jumamosi, Mwananchi Jumapili, Mwanaspoti, The Citizen na The Citizen on Sunday, Tido Mhando ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa MCL na Theophil Makunga, Meneja wa Uendeshaji na Biashara MCL.
Swali: Makao Makuu ya Serikali ya Muungano yatakuwa wapi?
Warioba: Ukibadili Katiba wakati wowote ni lazima kuwe na makubaliano fulani.
Unajua Serikali ya Muungano na Tanganyika ilikuwa pamoja, sasa ukianzisha Serikali ya Tanganyika, lazima kwenye mpangilio muanze kugawana hata wafanyakazi kwa kuwa wafanyakazi hao walikuwa ni wa Muungano. Hapo ndiyo mtaamua wafanyakazi gani watakwenda katika Serikali ya Tanganyika, watakaobaki katika Muungano na wale watakaokwenda Zanzibar.
Hata katika majengo hali inakuwa hivyo hivyo, lazima kutakuwa na majengo yaliyokuwa yakitumiwa na wizara mbalimbali na hata Ikulu. Hapo pia lazima myagawanye na kukubaliana viongozi wa Tanganyika watakuwa wapi na wale wa Muungano watakuwa wapi. Lakini, hata vifaa vya kutendea kazi navyo inatakiwa mgawane kulingana na makubaliano yenu.
Suala hili linategemea zaidi mazungumzo ya pande zote mbili, baada ya kukamilika kwa mchakato huu kwa sababu hii iliyopatikana sasa ni rasimu tu, ambayo itajadiliwa na wananchi kabla ya kuanza kwa Bunge la Katiba na baadaye kuwepo kwa kura ya maoni. Wapo watakaokuwa wakihoji kuhusu vyeo, katika hili itakuwa kama tulivyokuwa tukiungana Tanganyika na Zanzibar, wakati huo wapo ambao walikuwa wakuu wa mikoa na wakajikuta wameingia katika Muungano huku wakiwa na vyeo hivyo. Kilichofanyika ni kuendelea tu na nafasi hizo mpaka utakapofanyika utaratibu mwingine kwa njia ya mazungumzo.
Unajua jambo hili siyo jukumu la tume hii, tunaliacha kwa sasa na hatujui litakuwaje kwa sababu ni suala la mazungumzo.
Swali: Majukumu ya Rais yatakuwaje?
Warioba: Rasimu imeeleza majukumu (roles) ya Rais kama mkuu wa nchi, ambaye anakuwa kama taasisi na sisi tulichokifanya ni kujenga taasisi hizo, kwamba ijulikane akifanya chochote awe ameshauriwa, isiwe yeye peke yake.

Msanii bongo movie aliyeanza kucheza filamu Ulaya

Kama utakuwa shabiki na mtazamaji mzuri wa filamu za bongo movie, jina la Lucy Francis Komba halitakuwa jipya masikioni mwako.
 
Msanii huyu alianza sanaa katika Kundi la Kaole, akishiriki baadhi ya vipindi vya televisheni na baadaye kujiunga na Kikundi cha Dar Talent, ambapo alishiriki filamu moja ya vichekesho.
Katika sanaa, Lucy ameshacheza filamu zaidi ya 50 zikiwemo nne alizocheza nje ya nchi. Filamu ya kwanza aliyocheza nyota huyu na kuonyesha kipaji chake inafahamika kama Utata. Baadaye alishiriki filamu ya Yolanda, Division of Love, Jeraha la Ndoa, Talaka Wodini, Siri ya Moyo Wangu, Teke la Mama, Richmond, Swadakta na nyinginezo.
Kwa sasa Lucy ni mwigizaji wa filamu, mwongozaji, mtunzi wa stori na mtayarishaji wa filamu aliyefanikiwa kuvuka mipaka ya nchi hasa Bongo Movie akichanua hadi katika nchi za Burundi, Sierra Leone na Denmark.
Lucy kwa sasa anasubiri kuzindua filamu yake mpya aliyoichezea nchini Denmark.
”Nilienda kupumzika tu, lakini baada ya kuona wana mwitikio mzuri na filamu zetu, ilinibidi nicheze filamu niliyoipa jina la ‘Tanzania to Denmark’,” anasema Lucy.
Anabainisha kuwa filamu hiyo amecheza kwa gharama zake akishirikiana na Kampuni ya Vad Production ya Denmark inayojihusisha na uzalishaji wa filamu.
“Walinisaidia sana hadi hatua ya mwisho. Natarajia kuizindua mwezi huu wa Juni nchini Denmark, naamini itauza sana, maana nimecheza na wasanii maarufu wa huko,”anasema Lucy.
Aprili mwaka jana, msanii huyo alifanikiwa kwenda nchini Ghana kwa maandalizi ya kucheza filamu yake, hata hivyo hakuweza kufanikiwa baada ya msanii mwenzake Kanumba kufariki dunia.
“Mimi nilikuwa nimeshatangulia, nikiwa huko nikasikia amefariki ikanibidi nirudi kwanza nyumbani kwa mazishi yake,”anasema Lucy.
Kabla ya kuondoka Ghana, Lucy alibahatika kufanya mahojiano na mastaa wa nchini Sierra Leone waliokuwa wakikusanya washiriki wakubwa kwa lengo la kuandaa filamu itakayojitambulisha kimataifa.
Maandalizi hayo ni maarufu kama ‘famous film magazine in Africa’ ambayo imewashirikisha baadhi ya nyota akiwamo Van Vicker, Ini Edo, Desmond na wengineo katika kuandaa filamu ya ‘Repackage live’.

Friday, May 24, 2013

Prof Jay: Sitaki hata udiwani!

Dar. Msanii wa muziki wa kizazi kipya, Joseph Haule (Profesa Jay) amesema amejiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ili kukisaidia chama katika changamoto za kuikomboa nchi.
 
Akizungumza na Mwananchi jana Profesa J alisema hajajiunga na Chadema ili kugombea ubunge mwaka 2015, isipokuwa kwa dhumuni la kutaka kuongeza nguvu katika chama hicho akiwa kama kijana.
“Kujiunga na siasa si dhambi na haina maana kwamba nina mpango wa kugombea jimbo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015. Sihitaji kugombea hata udiwani ila ni kwa dhumuni la kutaka kuongeza nguvu katika chama ili kuyafikia malengo,” alisema.
Alisema yeye ni mfuasi wa Chadema tangu mwaka 2005 na amekuwa karibu na chama kwa nyakati nyingi lakini kwa sasa ameamua kuingia rasmi katika chama kama chachu katika kuongeza harakati kwa vijana.
“Nimeingia ili nisaidie hiki chama kuikomboa Tanzania kwani kwa muda mrefu niliokaa katika chama hiki nimegundua kuwa wamedhamiria kumkomboa msanii, kijana wa kawaida na wakubwa kwa wadogo hivyo nadhani nipo sahihi katika uamuzi wangu.”
“Natambua mimi ni mwanamuziki, sawa nina mashabiki wengi lakini haina maana kwamba sina haki ya kuchagua chama ninachoona mimi kinanifaa, lakini siwezi kusita kufanya kazi sehemu yoyote au wakati wowote chama kikinitaka nifanye kwa wakati husika,” alisema Profesa J.
Profesa J juzi alijiunga rasmi na chama hicho baada ya kukabidhiwa kadi ya Chadema mjini Dodoma na Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi akiwa sambamba na msanii mwingine wa hiphop Kulwa Kinega maarufu kama K wa Mapacha ambaye alikabidhiwa kadi hiyo na Mbunge wa Ubungo John Mnyika.

JWTZ wakanusha taarifa za askari kujihusisha na makahaba DRC

  Dar es Salaam. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania, JWTZ, limekanusha taarifa zilizotapakaa kwenye mitandao kuwa askari wa jeshi hilo waliokwenda huko kwa ajili ya kulinda amani,wameanza kujihusisha na makahaba.
 
Kwa mujibu wa taarifa ya Kurugenzi ya Habari na Uhusiano, Mtandao wa www.congodrcnews.com wanajeshi wa Tanzania wameanza kujihusisha na ubakaji wanawake katika Mji wa Sake ulioko Goma.
Taarifa hizo zimeeleza kuwa askari mmoja wa JWTZ alihitaji kujamiiana na mwanamke mmoja(Kahaba) kwa ujira wa Dola 50. Baada ya kumaliza shida zake ambazo ilielezwa alizifanya bila kinga yoyote,askari huyo alikataa kumlipa ujira wake,hali iliyoleta tafrani na mwanamke huyo kupiga kelele.
“JWTZ linapenda kuwaeleza wananchi kuwa taarifa hizo ni za uongo mtupu wenye nia ya kulipaka matope JWTZ na Tanzania kwa ujumla. “Picha iliyotolewa kwenye tovuti hiyo ya www.congodrcnews.com ni ya wanajeshi wa Tanzania walipokuwa katika Operesheni ya huko Comoro mwaka 2008.
Mtu anayeonekana kuwa chini ya Ulinzi alikuwa ni mshiriki wa Kanali Mohamed Bacar ambaye aliondolewa madarakani.
“Vilevile picha hiyo ilitolewa vile vile katika tovuti za www.apc.net.au/news/stories ya Machi 26, 2008 na ww.
Seattletimes.com. na pia picha hiyo ipo pia kwenye tovuti ya Jamii Forum baada ya kufanya ‘link’ kutoka kwenye Mtando wa www.google.com.”
Taarifa hiyo ilisema kuwa JWTZ inapenda kueleza wananchi na dunia kwa ujumla kwamba wanaoneza taarifa hizo wana lengo la kukatisha tamaa juhudi zinazofanywa na
nchi za Maziwa Makuu na SADC kuleta amani nchini DRC kwani JWTZ wako DRC kwa mujibu wa taratibu za kiutendaji za Umoja wa Mataifa. 

Sunday, April 7, 2013

PICHA ZA JINSI JAY Z NA BEYONCE WALIVYOREHEKEA MIAKA MITANO YA NDOA NCHINI CUBA NA KUPITA MITAANI


.
.
3
.
.
.
.
.
.
.
.
11
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.

Mwananchi yazoa tuzo za umahiri

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Seif Sharif Hamad (kushoto) akimkabidhi mfano wa hundi ya dola 4,000 za Marekani mshindi wa  jumla wa Tuzo ya Uandishi Bora, mwandishi wa gazeti la The Citizen, Lucas Liganga, wakati wa hafla ya utoaji wa tuzo hizo iliyoandaliwa na Baraza la Habari Tanzania (MCT) Dar es Salaam, juzi usiku. Picha  na  Emmanuel Herman 
Dar es Salaam: Waandishi wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) inayochapa magazeti ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti wameibuka tena kidedea kwenye tuzo  za umahiri wa Uandishi wa Habari Tanzania (EJAT) kwa mwaka 2012, baada ya kushinda tuzo 13, ikiwamo ya mshindi wa jumla.
Sherehe za utoaji wa tuzo hizo ilifanyika jana katika Ukumbi wa Diamond Jubilee na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwamo Makamu wa Kwanza wa Rais, Seif Sharif Hamad ambaye alimwakilisha Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein.
Mshindi wa jumla kwa mwaka 2012 ni Lucas Liganga wa gazeti la The Citizen, ambaye ameifanya MCL kunyakua tuzo hiyo kwa miaka miwili mfululizo ambapo mwaka 2011 tuzo hiyo ilichukuliwa na Neville Meena wa gazeti la Mwananchi.
Washindi walipewa zawadi za magodoro, televisheni, Ipad na vyeti, huku mshindi wa jumla akipewa dola 4,000 za kujiendeleza kimasomo.
MCL iliingiza fainali waandishi 14 kati ya 66 walioteuliwa kuwania tuzo hizo ambao ni pamoja na Samweli Mwamkinga, Florence Majani, Polycarp Machira, Tom Musoba, Elias Msuya, Leon Bahati, Lucas Liganga, Shija Felician, Fredy Azzah, Joseph Zablon, Zephania Ubwani, Tumaini Msowoya, Anthony Mayunga na Edward Qorro.
Mbali na kutoa mshindi wa jumla, waandishi sita wa magazeti hayo walikuwa ndio wagombea pekee wa tuzo mbili za habari bora ya Uchumi na Biashara na Majanga, huku Azzah akishinda tuzo ya habari bora ya Virusi vya Ukimwi (VVU) ambapo alikuwa peke yake na alichaguliwa mara mbili kuwania tuzo hiyo.
Waandishi wa MCL walioshinda na tuzo zao katika mabano ni Edward Qorro (Uchumi na Biashara), Lucas Liganga (Mazingira na Malaria), Fredy Azzah (Ukimwi na Elimu), Anthony Mayunga (Utawala Bora).
Wengine ni Florence Majani (Sayansi na Teknolojia na Afya ya Uzazi), Samwel Mwakibinga (Mchora katuni bora), Zephania Ubwani (Kilimo), Polycarp Machira (Majanga), Shija Felician (Tuzo ya wazi).
Katika tuzo ya jumla MCL iliingiza waandishi watatu kati ya waandishi wanane waliochaguliwa kuwania tuzo hizo ambao ni Lucas Liganga, Fredy Azzah na Florence Majani.
Katika utoaji wa tuzo hizo, MCL ilifuatiwa na Shirika la Utangazaji (TBC) ambalo lilizoa tuzo nane, Afya Redio (6) na Kilimanjaro Film Institute (5).
Tuzo ya Uchumi na Biashara kwa upande wa televisheni ilichukuliwa na John Lewanga wa TBC, tuzo ya michezo na utamaduni kwa upande wa magazeti ilichukuliwa na Abdul Mohammed wa gazeti la The African, Abdallah Majura wa ABM FM alishinda tuzo hiyo kwa upande wa redio.
Tuzo ya mazingira upande wa redio ilichukuliwa na Idd Juma Yusuf wa Afya Redio, tuzo ya afya upande wa magazeti ilichukuliwa na Beatrice Shayo wa Nipashe na upande wa redio ilichukuliwa na Gervas Hubile wa TBC-Taifa.
Tuzo za Ukimwi na VVU upande wa redio ilikwenda kwa Andrew Kiwanyi wa Kilimanjaro Film Institute.
Tuzo ya habari za watoto upande wa magazeti ilichukuliwa na Shadrack Sagati wa Habari Leo, upande wa Televisheni alichukua Daniel Kaminyoge wa Kilimanjaro Film Institute, upande wa redio ilichukuliwa na Mwamini Andrew wa TBC.
Utawala bora upande wa Televisheni ilichukuliwa na Jamal Hashim Said wa TBC, upande wa Redio ilichukuliwa na Noel Thompson wa Afya Redio.
Tuzo za habari za jinsia kwa upande wa magazeti ilichukuliwa na Husna Mohammed wa Zanzibar Leo, upande wa Televisheni tuzo hiyo ilichukuliwa na Bernard Mwaituka Televisheni Iringa.
Tuzo ya Sayansi na Teknolojia upande wa  televisheni ilichukuliwa na Rose Kibaja wa TBC na upande wa redio ilichukuliwa na Abel Onesmo wa Clouds FM.
Upande wa tuzo za habari za Majanga kwa upande wa redio alichukua Noel Thompson wa Afya Redio, habari za malaria kwa upande wa Televisheni alichukua Dotto Mnyadi wa TBC na upande wa redio ilichukuliwa na Faraja Sendegeya wa Afya Redio.