Tuesday, August 20, 2013

Viongozi wamtuhumu Mwigulu Nchemba kushirikiana na polisi kutisha wananchi.


0
Share


Singida. Polisi wametanda  eneo la mkutano  wa Baraza la Katiba lililoandaliwa na Chadema, Wilaya ya Iramba.
Mkutano huo ulifanyika juzi katika Uwanja wa Soko la Zamani, ambako ni nyumbani kwa Mbunge wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba. Baada ya kuwasili kwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa, askari walionekana kutanda kila kona ya uwanja huo.
Baadhi ya askari walikuwa wameshikilia mabomu ya machozi na marungu huku wakiwa wamevalia kofia ngumu,  lakini muda mfupi gari lililosheheni Polisi wa Kutuliza Ghasia (FFU) liliwasili  wanjani hapo na kuegeshwa pembeni mwa mkutano.
Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Mabere Marando,   alikuwa wa kwanza kupanda jukwaani na kukemea kitendo hicho.
“Ndugu zangu polisi mnatumika vibaya jinsi mlivyokaa hapa mkiwa mmevalia kofia zenu na mabomu kama vile mnataka kupambana na wahalifu, ni kitendo kibaya,” alisema Marando na kuongeza:
“Huu mkutano umeruhusiwa  kisheria na Tume na nyie hamna mamlaka ya kuuzuia,  ila nadhani haya ni maagizo kutoka kwa Mbunge Mwigulu Nchemba kama tulivyokuwa tumeelewa kabla ya kufika. “Naye Dk Slaa aliwataadharisha polisi kuacha tabia ya kufanya kazi zao kwa maelekezo ya watu, bila kufuata taaluma zao.
“Kila siku tunawalalamikia polisi kuwa chanzo cha vurugu, huu ni ushahidi tosha mmezunguka jukwaa langu lote huku wananchi ambao ni walengwa mmewasogeza mbali,” alisema Dk Slaa na kuongeza:
“Sikuja hapa kuongea na nyie, nimewafuata wananchi naomba mtoke mkae mbali ili watu wangu wasogee karibu na hiyo ni amri.”
Kitendo ambacho kilipokelewa kwa shangwe na wananchi kwa kushangilia na kuweza kusogea karibu ya jukwaa.

Ponda Dar mpaka Moro kwa Helikopta

Katibu wa Taasisi na Jumuiya za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda alisafirishwa jana kwa helikopta kutoka Dar es Salaam kwenda Morogoro na kupandishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Mkoa kujibu mashtaka yanayomkabili.
Ponda jana alianza kwa kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Kisutu asubuhi na kufutiwa mashtaka ya uchochezi yaliyokuwa yakimkabili baada ya kusomewa mara ya kwanza Agosti 14, mwaka huu akiwa kitandani katika Taasisi ya Mifupa ya Hospitali ya Muhimbili, baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), kuwasilisha hati ya kutokuwa na nia ya kuendelea kumshtaki.
Alidaiwa kutenda makosa hayo katika maeneo mbalimbali ya Jamhuri ya Muungano kati ya Juni 2 na Agosti 11 mwaka huu.
Ponda alifikishwa mahakamani hapo saa 12 asubuhi na baadaye alipandishwa kizimbani na kufutiwa kesi hiyo, baada ya Wakili Kweka kuwasilisha hati hiyo ya DPP chini ya Kifungu cha 91 (1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA).
Hata hivyo, baada ya kufutiwa mashtaka hayo, aliendelea kushikiliwa na kisha akachukuliwa na kupelekwa Morogoro ambako pia alisomewa mashtaka ya uchochezi.
Kuwasili Moro
Sheikh Ponda aliwasili kwa helikopta ya polisi na kutua kwenye Uwanja wa Gofu, Morogoro akiwa chini ya ulinzi wa polisi na alipakiwa kwenye gari maalumu ambalo liliongozana na magari mengine matatu ya polisi huku ulinzi ukiwa umeimarishwa katika eneo la Mahakama ukiwajumuisha askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), askari wa upelelezi, Usalama wa Taifa pamoja na mbwa wa polisi na kusababisha shughuli za kazi katika Mahakama hiyo na ofisi za jirani kusimama kwa muda.
Baada ya kufika mahakamani saa tano asubuhi, magari yalisimama kwa takriban dakika 30 kabla ya kumtoa na kumwongoza kwenye Mahakama ya wazi ambayo tayari ilikuwa umejaa watu.
Baada ya kumalizika kusomwa kwa kesi hiyo, msafara uleule ulimrejesha Uwanja wa Gofu saa sita mchana na kupandishwa kwenye helikopta kurejea Dar es Salaam.
Mahakamani Morogoro
Ponda alisafirishwa kwa helikopta ya polisi hadi Morogoro na kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mfawidhi akiwa chini ya ulinzi mkali.

Vigogo kutoa ushahidi dhidi ya Mbunge Lema

Arusha. Mkuu wa Chuo cha Uhasibu cha Arusha, John Nanyaro na Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Arusha, Gillis Mroto, leo wanaanza kutoa ushahidi katika kesi ya tuhuma za uchochezi inayomkabili Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema.
Mashahidi wengine katika kesi hiyo ni, Mkaguzi wa Polisi Bernard Nyambanyana na mwenzake aliyetajwa kwa jina moja la Jane.
Hali kadhalika PC Godfrey na Joachim Mahanyu . Wakili wa Serikali, Elinenya Njiro, alitaja mashahidi wengine watakaotoa ushahidi wao mahakamani kuwa Faraji Mnepe, Benjamin Simkanga na Naibu Hamidu, wote kutoka Chuo cha Uhasibu.
Lema anadaiwa kutoa maneno ya uchochezi kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magessa Mulongo, alikwenda katika Chuo cha Uhasibu cha Arusha, mithili ya mtu aliyekwenda kwenye send-off na kwamba hajui chuo hicho kilipo wala mauaji ya mwanafunzi wa chuo hicho.
Wakili Njiro alidai kuwa mbunge huyo alitenda kosa hilo Aprili 24 mwaka huu, akiwa katika eneo la Freedom Square ndani ya Chuo cha Uhasibu na kwamba kitendo hicho kinapingana na kifungu cha 390 sura ya 35 ya sheria ya kanuni ya adhabu.

Saturday, July 13, 2013

Vita kali Chadema, CCM

Vyama vya CCM na Chadema vimekuwa vikituhumiana kuhatarisha amani ya nchi
Dar es Salaam. Siku tatu baada ya Rais Jakaya Kikwete kuponda mpango wa Chadema kuanzisha kambi kwa ajili ya mafunzo ya ulinzi kuwalinda viongozi na wanachama wake,  chama hicho kikuu cha upinzani nchini kimeibuka na kusema kuwa kinaendelea na mpango huo na kambi hizo zitaanza rasmi wiki ijayo.
Kimesema hakitishwi na kauli ya Jeshi la Polisi kukionya juu ya  uanzishwaji wa mafunzo hayo,  kwamba jeshi hilo linatakiwa kuanza kukizuia Chama Cha Mapinduzi (CCM)  kwanza, kwa maelezo kuwa chama hicho tawala pia kina kikundi cha ulinzi ‘Green Guards’ ambacho kinafanya mafunzo ya kijeshi, huku kikitumia silaha za moto.
“CCM ndiyo wataipeleka nchi hii pabaya, wanawafundisha vijana huku wakiwabebesha  bunduki, wanajenga taifa la aina  gani, bunduki ni silaha ya kivita sasa wanaandaa watu kupigana na nani” alisema Mkurugenzi wa Organaizesheni na Mafunzo wa chama hicho, Benson Kigaira jana wakati akizungumza na wanahabari huku akionyesha picha za mafunzo ya CCM, zinazoonyesha vijana wakiwa wamebeba silaha (hata hivyo ni mbao zilizotengenezwa kwa mfano wa bunduki).
Wakati Chadema wakieleza hayo, CCM kimeshtushwa na taarifa hizo na kueleza kuwa hali hiyo sasa inahatarisha usalama wa nchi.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa chama hicho (UVCCM), Martin Shigela alisema ni vyema Chadema kikawaambia wananchi wawalinde, kuliko kuanzisha mafunzo huku akimtaka Msajili wa Vyama vya siasa nchini, John Tendwa kulitizama kwa kina suala hilo.
Akifunga Kongamano  la Amani lililoandaliwa  na Kituo cha Demokrasia  Tanzania (TCD), Dar es Salaam Julai 10, mwaka huu, Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Taifa pia alikosoa kitendo cha Chadema kususia kongamano hilo alisema, “Sasa hawa kweli wanapenda amani yetu wakati hawapendi tuzungumze wanataka watu wauane, wapigane.”
Mbali na Rais Kikwete, Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, SSP Advera Senso juzi alikionya chama hicho kuhusu mpango huo akisema kuwa kitendo cha chama chochote cha siasa kikiwemo Chadema, kuanzisha kikundi cha kujihami ni kinyume na sheria za nchi na endapo watafanya hivyo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
Kauli ya jana ya Chadema ni mwendelezo wa ile iliyotolewa na Mwenyekiti wa chama hicho Freeman Mbowe Julai 9, mwaka huu, ambapo alisema  kimechukua hatua hiyo baada ya Serikali na vyombo vyake vya ulinzi na usalama kushindwa kufanyia kazi malalamiko yao kuhusu mauaji, vitisho na matukio ya kutisha wanayofanyiwa baadhi ya viongozi na wanachama wao.
Katika ufafanuzi wake Kigaila alisema Chadema hakianzishi vikundi vya kijeshi, bali mafunzo ya  kuwafundisha walinzi wa chama hicho  ‘Red Brigade’, jinsi ya kujilinda.
“Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni haki kwa raia yeyote kujilinda, Chadema ni taasisi ni haki yetu kuilinda taasisi yetu ndiyo maana tumesajili kikundi chetu cha ulinzi, sasa nani anatutisha, tunataka polisi waanze na CCM kwanza ambao katika mafunzo yao  wanafundisha hadi kupiga saluti na kutumia silaha,” alisema.
Alisema mafunzo hayo yataanza rasmi wiki ijayo, huku akisita kutaja siku yatakayoanza, wala mikoa yatakayofanyika na kusisitiza kuwa hayo yatatangazwa wiki ijayo wakati vijana wakienda katika mafunzo.

Sunday, June 9, 2013

Warioba: Ikulu kugawanywa

Dar es Salaam: Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema iwapo Mfumo wa Serikali Tatu utaridhiwa na wananchi ni lazima mambo yaliyo ndani ya Muungano yatagawanywa ikiwa ni pamoja na Ikulu ya Rais.
Amesema kuwa kutokana na taifa kufanya mabadiliko ya Katiba ni lazima kuwepo mpangilio wa kugawana mambo mbalimbali yaliyokuwa chini ya Muungano ikiwamo majengo, wafanyakazi, Ikulu, hata vitendea kazi na kwamba utaratibu huo ni kama ule uliotumika wakati Tanganyika na Zanzibar zilipoungana.
Kauli ya hiyo ya Jaji Warioba imekuja siku tatu tangu Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe kueleza kuwa Tanzania Bara itaanza mchakato wa kutunga Katiba yake Aprili mwaka 2014 na kumalizika Desemba mwaka huohuo.
Jaji Warioba aliyasema hayo katika mahojiano maalumu na waandishi waandamizi wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), inayochapisha magazeti ya Mwananchi, Mwananchi Jumamosi, Mwananchi Jumapili, Mwanaspoti, The Citizen na The Citizen on Sunday, Tido Mhando ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa MCL na Theophil Makunga, Meneja wa Uendeshaji na Biashara MCL.
Swali: Makao Makuu ya Serikali ya Muungano yatakuwa wapi?
Warioba: Ukibadili Katiba wakati wowote ni lazima kuwe na makubaliano fulani.
Unajua Serikali ya Muungano na Tanganyika ilikuwa pamoja, sasa ukianzisha Serikali ya Tanganyika, lazima kwenye mpangilio muanze kugawana hata wafanyakazi kwa kuwa wafanyakazi hao walikuwa ni wa Muungano. Hapo ndiyo mtaamua wafanyakazi gani watakwenda katika Serikali ya Tanganyika, watakaobaki katika Muungano na wale watakaokwenda Zanzibar.
Hata katika majengo hali inakuwa hivyo hivyo, lazima kutakuwa na majengo yaliyokuwa yakitumiwa na wizara mbalimbali na hata Ikulu. Hapo pia lazima myagawanye na kukubaliana viongozi wa Tanganyika watakuwa wapi na wale wa Muungano watakuwa wapi. Lakini, hata vifaa vya kutendea kazi navyo inatakiwa mgawane kulingana na makubaliano yenu.
Suala hili linategemea zaidi mazungumzo ya pande zote mbili, baada ya kukamilika kwa mchakato huu kwa sababu hii iliyopatikana sasa ni rasimu tu, ambayo itajadiliwa na wananchi kabla ya kuanza kwa Bunge la Katiba na baadaye kuwepo kwa kura ya maoni. Wapo watakaokuwa wakihoji kuhusu vyeo, katika hili itakuwa kama tulivyokuwa tukiungana Tanganyika na Zanzibar, wakati huo wapo ambao walikuwa wakuu wa mikoa na wakajikuta wameingia katika Muungano huku wakiwa na vyeo hivyo. Kilichofanyika ni kuendelea tu na nafasi hizo mpaka utakapofanyika utaratibu mwingine kwa njia ya mazungumzo.
Unajua jambo hili siyo jukumu la tume hii, tunaliacha kwa sasa na hatujui litakuwaje kwa sababu ni suala la mazungumzo.
Swali: Majukumu ya Rais yatakuwaje?
Warioba: Rasimu imeeleza majukumu (roles) ya Rais kama mkuu wa nchi, ambaye anakuwa kama taasisi na sisi tulichokifanya ni kujenga taasisi hizo, kwamba ijulikane akifanya chochote awe ameshauriwa, isiwe yeye peke yake.

Msanii bongo movie aliyeanza kucheza filamu Ulaya

Kama utakuwa shabiki na mtazamaji mzuri wa filamu za bongo movie, jina la Lucy Francis Komba halitakuwa jipya masikioni mwako.
 
Msanii huyu alianza sanaa katika Kundi la Kaole, akishiriki baadhi ya vipindi vya televisheni na baadaye kujiunga na Kikundi cha Dar Talent, ambapo alishiriki filamu moja ya vichekesho.
Katika sanaa, Lucy ameshacheza filamu zaidi ya 50 zikiwemo nne alizocheza nje ya nchi. Filamu ya kwanza aliyocheza nyota huyu na kuonyesha kipaji chake inafahamika kama Utata. Baadaye alishiriki filamu ya Yolanda, Division of Love, Jeraha la Ndoa, Talaka Wodini, Siri ya Moyo Wangu, Teke la Mama, Richmond, Swadakta na nyinginezo.
Kwa sasa Lucy ni mwigizaji wa filamu, mwongozaji, mtunzi wa stori na mtayarishaji wa filamu aliyefanikiwa kuvuka mipaka ya nchi hasa Bongo Movie akichanua hadi katika nchi za Burundi, Sierra Leone na Denmark.
Lucy kwa sasa anasubiri kuzindua filamu yake mpya aliyoichezea nchini Denmark.
”Nilienda kupumzika tu, lakini baada ya kuona wana mwitikio mzuri na filamu zetu, ilinibidi nicheze filamu niliyoipa jina la ‘Tanzania to Denmark’,” anasema Lucy.
Anabainisha kuwa filamu hiyo amecheza kwa gharama zake akishirikiana na Kampuni ya Vad Production ya Denmark inayojihusisha na uzalishaji wa filamu.
“Walinisaidia sana hadi hatua ya mwisho. Natarajia kuizindua mwezi huu wa Juni nchini Denmark, naamini itauza sana, maana nimecheza na wasanii maarufu wa huko,”anasema Lucy.
Aprili mwaka jana, msanii huyo alifanikiwa kwenda nchini Ghana kwa maandalizi ya kucheza filamu yake, hata hivyo hakuweza kufanikiwa baada ya msanii mwenzake Kanumba kufariki dunia.
“Mimi nilikuwa nimeshatangulia, nikiwa huko nikasikia amefariki ikanibidi nirudi kwanza nyumbani kwa mazishi yake,”anasema Lucy.
Kabla ya kuondoka Ghana, Lucy alibahatika kufanya mahojiano na mastaa wa nchini Sierra Leone waliokuwa wakikusanya washiriki wakubwa kwa lengo la kuandaa filamu itakayojitambulisha kimataifa.
Maandalizi hayo ni maarufu kama ‘famous film magazine in Africa’ ambayo imewashirikisha baadhi ya nyota akiwamo Van Vicker, Ini Edo, Desmond na wengineo katika kuandaa filamu ya ‘Repackage live’.

Friday, May 24, 2013

Prof Jay: Sitaki hata udiwani!

Dar. Msanii wa muziki wa kizazi kipya, Joseph Haule (Profesa Jay) amesema amejiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ili kukisaidia chama katika changamoto za kuikomboa nchi.
 
Akizungumza na Mwananchi jana Profesa J alisema hajajiunga na Chadema ili kugombea ubunge mwaka 2015, isipokuwa kwa dhumuni la kutaka kuongeza nguvu katika chama hicho akiwa kama kijana.
“Kujiunga na siasa si dhambi na haina maana kwamba nina mpango wa kugombea jimbo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015. Sihitaji kugombea hata udiwani ila ni kwa dhumuni la kutaka kuongeza nguvu katika chama ili kuyafikia malengo,” alisema.
Alisema yeye ni mfuasi wa Chadema tangu mwaka 2005 na amekuwa karibu na chama kwa nyakati nyingi lakini kwa sasa ameamua kuingia rasmi katika chama kama chachu katika kuongeza harakati kwa vijana.
“Nimeingia ili nisaidie hiki chama kuikomboa Tanzania kwani kwa muda mrefu niliokaa katika chama hiki nimegundua kuwa wamedhamiria kumkomboa msanii, kijana wa kawaida na wakubwa kwa wadogo hivyo nadhani nipo sahihi katika uamuzi wangu.”
“Natambua mimi ni mwanamuziki, sawa nina mashabiki wengi lakini haina maana kwamba sina haki ya kuchagua chama ninachoona mimi kinanifaa, lakini siwezi kusita kufanya kazi sehemu yoyote au wakati wowote chama kikinitaka nifanye kwa wakati husika,” alisema Profesa J.
Profesa J juzi alijiunga rasmi na chama hicho baada ya kukabidhiwa kadi ya Chadema mjini Dodoma na Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi akiwa sambamba na msanii mwingine wa hiphop Kulwa Kinega maarufu kama K wa Mapacha ambaye alikabidhiwa kadi hiyo na Mbunge wa Ubungo John Mnyika.