
YAMETIMIA. Safari ya miaka saba ya Baba Mtakatifu Benedict XVI
inakamilika leo pale atakapong’atuka rasmi katika uongozi wa Kanisa
Katoliki, ifikapo saa 2:00 usiku kwa saa za Italia (saa 4:00 usiku kwa
saa za Tanzania).
Kwa siku mbili, Papa amekuwa na shughuli
nyingi katika makao yake, Gandolfo Castel, Vatican akijiandaa kimwili
kuondoka, akiweka sawa nyaraka zake binafsi na zile za kanisa ambazo
zitawekwa katika kumbukumbu.
Kwa upande mwingine Vatican, nchi ambayo ipo
ndani ya Jiji la Rome iliyozungukwa na ukuta, ikiwa na ukubwa wa hekta
44 na wakazi 832 pekee, imekuwa katika hekaheka nyingi.
Jana, waumini
zaidi ya 50,000 na wengine wengi kutoka sehemu mbalimbali duniani
wakiwamo makardinali, maaskofu, mapadri na walei walialikwa kwa shughuli
rasmi ya kumuaga kiongozi huyo.
Tofauti na kanuni yake, leo Benedict hatavaa
viatu vyekundu kama ilivyozoeleka na badala yake amechagua viatu rahisi
vya ngozi vilivyobuniwa Mexico. Alipewa viatu hivyo ikiwa ni zawadi
wakati wa ziara nchini humo 2012.
Tangu alipotangaza uamuzi wake wa kung’atuka
Februari 11, mwaka huu, utata umegubika nafasi yake katika maisha mapya
ndani ya Vatican, akiitwa Papa Mstaafu.
Waumini, wataalamu na hata viongozi mbalimbali
wa Kikatoliki wameanza kuhoji ni jinsi gani viongozi wawili (Papa)
wataishi, huku wote wakivaa mavazi meupe wakiitwa Papa, wakiishi umbali
mdogo kati yao, wakiwa na wasaidizi wengi wanaowahudumia.
Vatican
Nje ya Gandolfo Castel, ulinzi umeimarishwa na vibali vya kuingia Vatican vimesitishwa.
Juzi,
Vatican ilitangaza kwamba Papa Benedict XVI atajulikana kama ‘Emeritus
Pope’, yaani Papa Mstaafu mwenye cheo cha heshima, akiendelea kuitwa,
‘mtakatifu’ na ambaye ataendelea kuvaa nguo nyeupe.
Mavazi na hata jina lake jipya ni masuala
ambayo yamezua uvumi mwingi, huku suala la mrithi wake mpya pia likiwa
gumzo, kwani tukio kama hilo lilitokea miaka 600 iliyopita.
Ni uamuzi
uliolishtua kanisa hilo lenye waumini 1.2 bilioni duniani na wengi
wanasema awali, haikushauriwa Papa kustaafu kwani kwa kufanya hivyo
kunaacha mizozo na minong’ono ya kuwania madaraka.
Hata hivyo, uongozi wa Vatican umesisitiza
kuwa uamuzi huo wa Papa Benedict XVI ni wa kipekee na hakuna mzozo ambao
utatokea baina yake na mrithi wake ambaye mchakato wa kumpata
unatarajiwa kuanza ndani ya wiki mbili zijazo.
“Kulingana na mabadiliko katika kanisa letu,
kuna Papa mmoja. Ni dhahiri kwamba katika hali ya sasa hakutakuwa na
tatizo,” anasema Mhariri wa Gazeti la L’Oservatore Romano linalomilikiwa
na Vatican, Giovanni Maria Vian.
Hofu iliyopo
Hata hivyo,
wakosoaji wa mambo hawakubaliani na hoja hiyo na baadhi ya makardinali
walioko Vatican kwa usiri mwingi, wanazungumzia suala hilo wakieleza
kwamba litazua tatizo kubwa kwa Papa ajaye, hasa ikiwa mtangulizi wake,
Benedict akiwa bado hai.
Mtaalamu wa tauhidi (theolojia), raia wa
Uswisi, Hans Kueng ambaye amekuwa mtu wa karibu wa Papa Benedict XVI,
ingawa kwa sasa ni mkosoaji wake amesema:
“Kwa sasa, Benedict XVI
akiwa bado hai, kuna hatari ya kuwa na Papa kivuli, mwenye mamlaka
kamili ambaye kwa chinichini anaweza kumshinikiza mrithi wake kufikia
uamuzi.”
Hans Kueng alisema hayo alipozungumza na Gazeti la Der Spiegel la Ujerumani.
Msemaji wa Vatican, Padri Federico Lombardi
alisema Papa Benedict XVI kwa upande wake aliamua aitwe Papa Mstaafu au
‘kiongozi mstaafu wa Roma.’ Anasema haelewi ni kwa nini ameamua kuacha
jina lake la sasa la Askofu wa Rome.
Kwa wiki mbili zilizopita, maofisa mbalimbali
wa Vatican wamekuwa wakifikiri kwamba Papa angeanza kuvaa mavazi meusi
na kutumia jina la Askofu Mstaafu wa Rome ili kuepuka mkanganyiko na
mrithi wake.