Taarifa hiyo pia ilisema mtu aliyekuwa na Dk Ulimboka kabla ya kukamatwa
 kwake alitambulishwa kwao na kigogo ambaye hakumtaja jina, kwa 
makubaliano kuwa atakuwa anachukua madai ya madaktari dhidi ya Serikali.“Nathibitisha
 kwamba mfanyakazi huyu wa Ikulu, ndiye aliyenipigia simu na kuniita 
kwenye kikao ambako muda mfupi baadaye nilitekwa,” inaeleza taarifa 
hiyo  na kuonyesha namba za simu za mtu huyo anayedaiwa ni mfanyakazi wa
 Ikulu.“Ninamfahamu sana bwana (jina tunalihifadhi kwa sasa),  
kwa sababu alikuwa akitumwa mara kwa mara kuja kukutana na mimi na 
tumekutana mara kadhaa kabla ya tukio lile. Nakumbuka alitambulishwa 
kwetu na kigogo mmoja nikiwa pamoja na wawakilishi wengine wa 
madaktari,” alisema.
Katika taarifa hiyo iliyoainisha namba 
iliyokuwa inatumiwa na Dk Ulimboka kuwasiliana na mtu huyo, inaeleza pia
 kuwa mpaka sasa mtu huyo yupo hai na kuwa yupo tayari kutoa ushirikiano
 kwa chombo huru ili kuhakikisha haki inatendeka.Taarifa 
inaeleza pia kuwa kwa nyakati tofauti mtu huyo alikuwa akitumwa kwa Dk 
Ulimboka na mtu ambaye tamko hilo halikumtaja, lengo likiwa ni kuchukua 
nyaraka mbalimbali na vyeti vya kuthibitisha taaluma za masomo yake.“Wale
 wote waliotuhumiwa na ninaowatuhumu kunitendea unyama huu wako huru na 
hakuna aliyeguswa. Je uhai na maisha yangu, yana thamani ndogo kama ya 
mnyama anayekwenda machinjioni? alihoji Dk Ulimboka katika taarifa hiyo 
na kuendelea:"Je Serikali ya nchi yangu itakubali lini kuundwa kwa tume huru kuchunguza unyama huu na kuhakikisha kuwa haki inatendeka?”
Dk
 Ulimboka amesema katika taarifa hiyo kuwa: “Niko tayari kuhojiwa na 
kutoa ushirikiano wangu kwa vyombo huru na makini vya uchunguzi ambavyo 
vitaundwa ili kuweza kuubaini ukweli.”
Maelezo ya wakili wake
Akisoma
 taarifa hiyo jana, Kicheere alisema kwa sasa Dk Ulimboka yupo nje ya 
nchi kwa matibabu zaidi na aliandika tamko hilo mbele ya Wakili Nshala, 
ambaye pia ameweka saini na mhuri wake.Hata hivyo, tamko hilo 
ambalo Kicheere alilisoma mbele ya waandishi wa habari jijini Dar es 
Salaam jana, linaonyesha lilitolewa Oktoba 7, mwaka 2011, jambo ambalo 
Nshala akizungumza na gazeti hili alisema ni makosa ya uchapaji.“Hilo tamko lilisomwa mbele yangu Oktoba 7, mwaka huu, hiyo ya kuandikwa mwaka 2011 ni makosa ya uchapaji tu.” alisema Nshala.Naye
 Kicheere alisema, Dk Ulimboka yupo tayari kusema ukweli wote wa 
kilichomkuta endapo itaundwa tume huru ya kuchunguza tukio hilo.
Alisema
 taarifa ambazo alizitoa na kurekodiwa kwenye vyombo mbalimbali vya 
habari ikiwamo mtandao ya kijamii, ni za kweli na alizotoa akiwa na 
akili na kumbukumbu nzuri.Tamko hilo linaeleza kwamba, moja ya 
uthibitisho kuwa taarifa hizo alizozitoa kabla ya kufika kwenye 
Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Kitengo cha Mifupa (Moi), na zile 
alizozitoa akiwa hapo, ni kule kuweza kumwita na kumshawishi mtu 
aliyemsaidia kutoka Msitu wa Pande.“Uthibitisho wa kumbukumbu 
nzuri niliyonayo, ni pale nilipokutana na  Juma Mganza katika Msitu wa 
Mabwepande asubuhi ya siku ya tukio. Pamoja na maumivu makali niliokuwa 
nayo kutoka kila sehemu ya mwili wangu, niliweza kumshawishi  Mganza 
kunifungua kamba za mikono nilizokuwa nimefungwa,” alisema Dk Ulimboka 
na kuongeza;
“Pia kukumbuka namba ya simu ya rafiki yangu Dk  
Deogratias ambapo  Mganza aliweza kuitumia kuwasiliana naye kumpa 
taarifa kuhusu tukio hilo. Ni kupitia taarifa hiyo ndipo suala la mimi 
kufikishwa Moi lilipofikiwa.”Aliendelea: “Na kama  niliweza 
kukumbuka namba ya rafiki yangu, mambo hayo yanatosha kuthibitisha kuwa 
ninachokisema ni ukweli na kuwa utimamu na kumbukumbu zangu ni sahihi”.
Usiku
 wa Julai 26,  mwaka huu, Dk Ulimboka alitekwa na watu wasiojulikana na 
kupigwa vibaya ambapo Julai 27, alikutwa kwenye Msitu wa Pande uliopo 
Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam.Baada ya tukio hilo, alisafirishwa mpaka Moi ambapo baadaye alipelekwa nje ya nchi kwa matibabu.
 
 
 
 

 
No comments:
Post a Comment