Tuesday, August 20, 2013

Ponda Dar mpaka Moro kwa Helikopta

Katibu wa Taasisi na Jumuiya za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda alisafirishwa jana kwa helikopta kutoka Dar es Salaam kwenda Morogoro na kupandishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Mkoa kujibu mashtaka yanayomkabili.
Ponda jana alianza kwa kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Kisutu asubuhi na kufutiwa mashtaka ya uchochezi yaliyokuwa yakimkabili baada ya kusomewa mara ya kwanza Agosti 14, mwaka huu akiwa kitandani katika Taasisi ya Mifupa ya Hospitali ya Muhimbili, baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), kuwasilisha hati ya kutokuwa na nia ya kuendelea kumshtaki.
Alidaiwa kutenda makosa hayo katika maeneo mbalimbali ya Jamhuri ya Muungano kati ya Juni 2 na Agosti 11 mwaka huu.
Ponda alifikishwa mahakamani hapo saa 12 asubuhi na baadaye alipandishwa kizimbani na kufutiwa kesi hiyo, baada ya Wakili Kweka kuwasilisha hati hiyo ya DPP chini ya Kifungu cha 91 (1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA).
Hata hivyo, baada ya kufutiwa mashtaka hayo, aliendelea kushikiliwa na kisha akachukuliwa na kupelekwa Morogoro ambako pia alisomewa mashtaka ya uchochezi.
Kuwasili Moro
Sheikh Ponda aliwasili kwa helikopta ya polisi na kutua kwenye Uwanja wa Gofu, Morogoro akiwa chini ya ulinzi wa polisi na alipakiwa kwenye gari maalumu ambalo liliongozana na magari mengine matatu ya polisi huku ulinzi ukiwa umeimarishwa katika eneo la Mahakama ukiwajumuisha askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), askari wa upelelezi, Usalama wa Taifa pamoja na mbwa wa polisi na kusababisha shughuli za kazi katika Mahakama hiyo na ofisi za jirani kusimama kwa muda.
Baada ya kufika mahakamani saa tano asubuhi, magari yalisimama kwa takriban dakika 30 kabla ya kumtoa na kumwongoza kwenye Mahakama ya wazi ambayo tayari ilikuwa umejaa watu.
Baada ya kumalizika kusomwa kwa kesi hiyo, msafara uleule ulimrejesha Uwanja wa Gofu saa sita mchana na kupandishwa kwenye helikopta kurejea Dar es Salaam.
Mahakamani Morogoro
Ponda alisafirishwa kwa helikopta ya polisi hadi Morogoro na kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mfawidhi akiwa chini ya ulinzi mkali.

No comments:

Post a Comment