Wednesday, February 19, 2014

Matokeo haya ya udiwani, wapinzani wajitafakari

Uchaguzi wa madiwani uliofanyika hivi karibuni katika kata 27 nchini, umezua majonzi ndani ya vyama vya upinzani, na hasa Chadema baada ya kuambulia kata tatu.
Licha ya vyama vingine vya upinzani kikiwemo Chama cha Wananchi (CUF) kukosa kabisa hata kata moja, huku NCCR-Mageuzi kikifanikiwa kutetea kata yake moja mkoani Kigoma, Chadema kinaugulia zaidi kutokana na nguvu iliyotumika dhidi ya CCM.
Kwanza Chadema kilisimimamisha wagogombea katika kata 26 kikilinganishwa na CCM iliyosimamisha wagombea katika kata zote 27. Mgombea mmoja wa Chadema alijitoa dakika za mwisho mkoani Tanga.
Isitoshe, uchaguzi huo umekuja wakati Chadema ikiwa katika Pperesheni Pamoja Daima (OPD) ambapo viongozi wa Taifa wa chama hicho wakiongozwa na Mwenyekiti, Freeman Mbowe na Katibu, Willibrod Slaa walishiriki.
Operesheni hiyo ilikuwa katika misafara ya helkopta tatu zikiwa zimesheheni makada wa chama hicho wakishambulia kwa zaidi ya mikutano 80 nzani ya wiki mbili.
Hata hivyo, operesheni hiyo ilionekana kufukiza ubani kutokana na mgogoro uliokuwa ndani ya chama hicho ambapo aliyekuwa Naibu Katibu wa chama hicho, Zitto Kabwe ambaye alivuliwa nyadhifa zake na kukimbia mahakamani kupinga hatua hiyo, huku wenzake aliyekuwa mjumbe wa Kamati Kuu, Dk Kitila Mkumbo na aliyekuwa Mwenyekiti mkoani Arusha, Samson Mwigamba wakifukuzwa uanachama.
Mbali na mikutano hiyo iliyokusanya watu wengi, Chadema iligusia masuala ya kitaifa na baadaye kujikita kwenye kata zenye uchaguzi na kupiga kampeni kwa wagombea wao.
Baada ya uchaguzi huo kufanyika Februari 9, matokeo yalionyesha kuipa CCM ushindi mkubwa katika kata 23.
Chadema kimeambulia kata tatu ambazo ni Sombetini, Arusha na Njombe mjini zilizokuwa za CCM na kutetea yak wake ya Kiborloni, Moshi.
Chama hicho kimepoteza kata zake za Bunda na Kigoma zilizokwenda CCM.
Uchaguzi huo ndio ulikuwa kipimo cha kukubalika kwa chama hicho hasa baada ya kutoka kwenye mgogoro wa ndani na huenda mgogoro uliokuwapo umekitikisa, hasa kutokana na baadhi ya viongozi wa mikoa na wilaya nao kuonyesha kuunga mkono kambi ya Zitto.

Ofisa habari wa chama hicho chadema, Tumaini Makene anasema licha ya kushinda kata tatu kati ya 27 chama hicho kimetoa upinzani wa kweli kwa kusimamisha wagombea kata 26, zikiwamo ambazo hakikuwa na nguvu, lakini kikapata kura nyingi.
Anasema wanaolinganisha matokeo hayo ya udiwani na mikutano ya chama hicho ya OPD iliyofanyika hivi karibuni, wanatakiwa kuangalia kura ambazo wagombea wa chama hicho wamepata.
“Wanaosema hayo, wamepotoka na hizo ni propaganda nyepesi,” inasema sehemu ya taarifa ya Makene.
Anasema lengo la mikutano ya OPD ilikuwa ni kuzungumzia mchakato wa Katiba Mpya, uboreshaji daftari la wapigakura, kuzungumzia rasilimali za nchi na ugumu wa maisha unaosababishwa na sera mbovu za CCM.
“Operesheni Pamoja Daima imeibua mambo mengi; Katiba Mpya, rasilimali za nchi na ugumu wa maisha unaowakabili wananchi na suala la daftari la wapigakura mpaka kufikia hatua na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kutangaza kulifanyia maboresho,” anasema.
Anasema maeneo ambayo mwaka 2010 hawakusimamisha mgombea udiwani wala mbunge, wamepata kura nyingi.
Chaguzi zilizopita
Tangu uliporudishwa mfumo wa vyama vingi, CCM bado imeonekana kuwa na nguvu hasa vijijini kutokana na muundo wake.
Licha ya kushinda katika chaguzi kuu, CCM imekuwa ikishinda vizuri katika chaguzi za Serikali za mitaa.
Kwa mfano katika uchaguzi wa mwaka 2009, CCM ilishinda viti vya wenyeviti wa vijiji na mitaa 264,344 sawa na asilimia 93.86, kikifuatiwa na CUF kilichopata viti 8,034 sawa na asilimia 2.85, wakati Chadema kilipata viti 6,480 sawa na asilimia 2.28.
Vyama vingine vilivyoshiriki ni pamoja na United Democratic (UDP) kilichopata viti 1,434 sawa na asilimia 0.51, NCCR-Mageuzi viti 614, asilimia 0.22, TLP 570, sawa (0.2 %), Chausta 158 (0.06), UPDP (25), PPT Maendeleo (12), NRA (4), DP (3), SAU (3) na UMD viti viwili.

No comments:

Post a Comment